Kuna mwanamuziki mmoja mtanzania, kati ya wale wanaoitwa wa kizazi kipya anatamani mambo ya kuchekesha sana katika moja ya nyimbo zake. Kwa mfano anatamani mlima Kilimanjaro uamie sijuhi wapi na bahari pia ihame. Mimi leo nakuwa kama yeye. Natamani Kipindupindu kilipuke Mikocheni, Osterbay, Masaki halafu kipige hodi Ikulu pia. 

Kila siku kinavamia Buguruni, Manzese na sehemu zingine za walalahoi. Hivi kweli tumeshindwa kabisa kudhibiti kipindupindu? Labda kikifika ikulu kitapatiwa ufumbuzi. Rais mpya kaanza kazi kwa kukaribishwa na mlipuko wa kipindupindu kama ilivyo kawaida ya kila mwaka. Sijuhi kama atakivalia njuga kwa Ari Mpya, Kasi Mpya na Nguvu mpya au kitaendelea kumaliza watu kwa Ari Mpya, Kasi Mpya na Nguvu Mpya? Kama waziri wa Afya ataendeleza mapambano ya magonjwa kwa warsha, semina na makongamano na kuchapisha fulana na kofia basi hakuna kitakachotokea. Safari hii Waziri wa Afya ni Profesa. Sijuhi kama atasadia lolote kwa sababu huko nyuma alishawahi kuwepo Profesa akaboronga pia. Mimi sijui aibu hii ya kipindupindu itaisha lini.

hii ni moja ya makala ambayo nilitokea kuipenda sana wakati naanza kublog miaka 8 iliyopita, ni moja ya makala za Ndesanjo Macha.Natamani sana kaka Ndesanjo uendelee na Mada Chokonozi kama hizi. 

photo







MJUMBE wa Baraza Kuu la Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) taifa, kupitia Mkoa wa Arusha, Benson Mollel (26) amekutwa amefariki dunia ndani ya Hoteli ya Lush Garden Business, iliyopo Mtaa wa Jacaranda katikati ya Jiji la Arusha.

Mashuhuda wa tukio hilo walisema Mollel alikutwa akiwa amekufa jana mchana na kwamba tukio hilo limezua hofu kwa wakazi wa Jiji la Arusha, huku wakijiuliza chanzo cha kifo chake.

Kifo cha mwanasiasa huyo mchanga ambaye pia alikuwa ni mfanyabiashara wa madini mkoani hapa, kimezusha maswali mengi wakati wengine wakihusisha tukio hilo na masuala ya kisiasa na upande mwingine wakidai ni masuala la kibiashara.

Hisia hizo zinatokana na ukweli kwamba Arusha ni jiji lenye hekaheka za kisiasa hasa ndani ya CCM ambapo Mollel alikuwa mmoja wa vinara wake.

Polisi waliwasili hotelini hapo saa 8.00 mchana na kuupakia mwili wa marehemu kwenye gari na kisha kuupeleka Hospitali ya Mount Meru kwa ajili ya kuhifadhiwa.

Mkuu wa Polisi wa Wilaya wa Arusha (OCD), Gilles Muruta akizungumza katika eneo la tukio alisema: “Tunachunguza tukio hili ambalo ni la ghafla.”

Akizungumzia kifo hicho, Katibu Mkuu wa UVCCM, Martin Shigela alisema: "Tumepokea kwa masikitiko kifo cha Mollel japokuwa sifahamu nini hasa kimejiri huko."

"Kuna rafiki yake alinipigia simu kuniarifu kuhusu kifo hicho na nikawaambia kama UVCCM Taifa tupate maelezo kamili na tujue nini cha kufanya. Iwapo familia itakuwa na mipango yoyote watutaarifu," alisema Shigela.


Baadhi ya wanasiasa na wafanyabiashara wa madini mkoani Arusha walionekana nje ya hoteli hiyo baada ya taarifa za kifo hicho kusambaa na wengine walishindwa kujizuia kisha kuangua vilio.

Miongoni mwao ni kada wa Chadema, James ole Millya na diwani wa CCM Kata ya Mlangarini, Mathias Manga. Katibu Mwenezi wa CCM wa Mkoa wa Arusha, Isaack Kadogoo ambaye pia alifika eneo hilo alisema kwamba wamepokea taarifa za tukio hilo kwa mshtuko mkubwa.

Uongozi wa hoteli hiyo haukuwa tayari kulizungumzia kwa madai kwamba limefikishwa katika vyombo vya usalama.

Hata hivy, kwa mujibu wa vyanzo vya habari ndani ya hoteli hiyo vilidai marehemu aliwasili usiku, juzi Jumamosi hotelini hapo akiongozana na mwanamke aliyetambulika kwa jina la Nancy na kuchukua chumba namba 208.
Mmoja wa walinzi hotelini hapo aliyetembulika kwa jina la Obeid Mollel kutoka Kampuni ya Ulinzi ya Victoria Support Services, alisimulia kuwa marehemu aliingia na mwanamke huyo na kisha kuondoka ghafla kabla ya kurejea tena wakiwa wote usiku.

Alisema kuwa wakati wakiwa hotelini hapo marehemu aliomba kuegesha gari lake jipya aina ya Mark II Grande ambalo halijasajiliwa na kwamba alipokubaliwa alifanya hivyo kisha akaenda chumbani. Ilibainika kuwa mwanamke huyo aliondoka jana asubuhi.

Taarifa zaidi
Mmoja wa wahudumu hotelini hapo (jina lake limehifadhiwa), alisema kuwa mwanamke aliyejitambulisha kwa jina la Mariam aliwasili hotelini hapo saa 5.00 asubuhi na kuomba kupelekwa moja kwa moja chumba alichokuwapo marehemu.

Mhudumu huyo alisema wakati mwanamke huyo akiomba kupelekwa chumbani, marehemu naye alipiga simu mapokezi akiomba mwanamke huyo apelekwe chumbani kwake, agizo ambalo walilitekeleza.

Kwa mujibu wa mhudumu, baadaye kama saa 6.00 mchana walimwona mwanamke huyo akitoka nje ya hoteli hiyo na kuondoka.
Alisema kwamba baadaye waliamua kupiga simu ya chumba alichofia marehemu ili kujua endapo ataendelea kupanga kwani muda wa kawaida ulikuwa umemalizika lakini simu hiyo ilikuwa ikiita bila majibu.

Mmoja wa wahudumu ambaye alikuwa akifahamiana na marehemu, aliamua kumpigia kupitia simu yake ya mkononi lakini nayo haikupokewa.

Mhudumu huyo aliamua kupanda ngazi kwenda chumbani kwa marehemu na katika hali isiyo ya kawaida alikuta mlango ukiwa wazi na marehemu akiwa amelala.

"Nilijaribu kumwamsha, lakini hakuamka na ndipo alipotoa taarifa kwa uongozi wa hoteli na baadaye waliviarifu vyombo vya usalama.

Chanzo cha kifo hiki kinakanganya maana kama kweli ni mauaji basi yamefanyika kwa ustadi mkubwa,” alisema mhudumu huyo na kuongeza:

“Unajua vyumba vyote vya huko juu ghorofani ukifunga mlango tu huku chini sisi mapokezi tunasikia, sasa cha ajabu mlango tumeukuta wazi. Hapa kuna maswali mengi," alieleza mhudumu huyo.


Mbunge wa kuteuliwa, mh.James Mbatia, amegomea uteuzi uliofanywa na waziri mkuu, Mizengo Pinda na kutaja sababu tatu za kukataa kushiriki katika tume iliyoundwa kuchunguza matoke mabaya ya kidato cha nne ya mwaka 2012.

Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana,Mbatia alisema amegomea uteuzi huo kwasababu tatu.

Mosi ni kwamba hajapata barua rasimi ya uteuzi,lakini pia ana hoja bungeni ambayo haijafika mwisho na tatu haiungi mkono tume hiyo.

Wakati huo huo,taarifa ya waziri mkuu alioitoa jana wakati akitangaza wajumbe wa tume hiyo inaonyesha kuwa ufaulu umeshuka toka asilimia 89 mwaka 2005 mpaka ailimia 43 mwaka 2012.

Kwa maneno memgine, tangu Kikwete aingie madarakani ufaulu umeshuka toka asilimia 89 mpaka asilimia 43.

Source:Tanzania Daima online la tarehe 03/03/2013.

Updates:
Gazaeti la habari leo online nalo pia linaripoti ya kuwa katibu mkuu wa chama cha walimu Tanzania, CWT, bwana Ezekiel Oluoch, ambae nae ameteuliwa kuwa mjumbe wa tume hiyo nae amekata uteuzi huo kwa kwasilisha barua ya kujitoa katika ofisi ya waziri mkuu.

Pia,gazeti hilo limefafanua ya kuwa habari za uhakika zinasema mh. Mbatia alipigiwa simu na katibu mkuu ofisi ya waziri mkuu, bwana Penniel Lyimo, akachukue barua yake ya uteuzi kama wenzake lakini hata hivyo mh.Mbatia hakuitikia wito huo.

Source:Habari leo online
.





Ilikuwa siku mbaya kwa Mfanyabiashara Ahmed Amran raia wa pakistan na wenzake watano walipofikishwa mbele ya mahakama ya hakimu Mkazi jjijini arusha kwa tuhuma za kutrosha nje ya nchi wanyamapori hai 136 wa aina 14 tofauti wenye thamani ya shilingi za kitanzania milioni 170. Kati ya watuhumiwa hao wawili kati yake walikuwa ni maafisa usalama wa uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kilimanjaro. Miongoni mwa wanyama wanaotuhumiwa kuwasafirisha ni pamoja na twiga, mnyama ambaye ni moja ya kielelezo cha nembo ya taifa


Maswali mengi yalioulizwa miongoni mwa wananchi ni kwa namna gani watuhumiwa hao waliweza kumsafirisha myama mrefu kama twiga ndani ya ndege mpaka Pakistan pasipo wana usalama lukuki waliopo uwanjani hapo kujua. Kitendo hicho ni ushahidi mzuri tu kuwa taifa letu sasa limegubikwa na ugonjwa hatari wa upungufu wa kinga za uchumi. Maliasili zinaibiwa na hakuna mtu anayejali zaidi ya viongozi kuendelea kuimba wimbo wa nchi yetu masikini. Mabilioni ya fedha yanakombwa pale benki kuu ya taifa lakini pasipo aibu bado viongozi wanaendelea kuimba wimbo wa Nchi yetu ni masikini. 


Kwenye madini nako wanakomba madini na kama hiyo haitoshi wanabeba mpaka mchanga na kuusafirisha nje ya nchi kwa ndege kupeleka kwao na bado viongozi wanaendelea na wimbo ule ule wa nchi yetu bado ni masikini. Ama kwa hakika taifa linaangamia, linaangamia kwa upungufu wa kinga za kiuchumi na ndio maana viongozi wanapata jeuri ya kuuza mpaka mbuga zetu za wanyama, fukwe za bahari, wamebakiza kuuza mito, maziwa na milima, tusipochukua hatua za kuwakemea hadharani watauza nchi nzima


Nchi yetu ina utajiri wa kutisha mfano wake hakuna duniani. Mungu aliijaza nchi yetu kwa madini ya thamani kubwa katika ardhi yake na juu yake akajaza milima ya kuvutia, mito itiririshayo maji, viumbe wa kila aina waishio majini na nchi kavu, mbuga za kuvutia zenye wanyama wa kila aina ambao wengine duniani hakuna, misitu ya kijani na mabonde ya kuvutia lakini bado wananchi wake wanaishi katika wimbi kubwa la umasikini.


Nchi yenye misitu na miti ya kila aina lakini watoto wake bado wanakaa chini kwa ukosefu wa madawati. Nchi yenye vyanzo vya maji kila mahali lakini wananchi wake hawana maji safi na salama ya kunywa.


Wakati nchi ikielekea kusimama huku bei za bidhaa zikipaa na kufanya hali ya maisha kuwa ngumu, viongozi wa nchi wanafanya sherehe na familia zao na kufuja mabilioni ya fedha za wananchi bila woga. Wenye akili timamu hawawezi kusherehekea miaka hamsini ya ndoa yao yenye matatizo lukuki huku watoto wao wakiwa katika hali ya mnuno mkali. Huu si wakati tena wa kusherehekea, ni wakati wa kuomboleza, ni wakati wa kufunga na kuliombea taifa litoke katika ugonjwa huu hatari. Ni wakati wa waumini wa dini zote bila kujali tofauti zao za kiimani kuyakemea mashetani yanayorudisha nyuma maendeleo ya wananchi

(Maelezo zaidi yanapatikana ndani ya kitabu changu cha Shukrani kitakachozinduliwa mwishoni wa mwezi wa tatu wamaka 2013)


Kwanza Records ni studio ya kisasa iliyopo Morogoro mjini ambayo kazi zake zimekuwa zikifanya vizuri katika uimwengu wa muziki wa kizazi kipya. Kwa mara ya Kwanza Studio ya Kwanza Records ilifanikiwa kumtambulisha katika anga la Muziki wa Bongo Fleva Msanii na Mchekeshaji maarufu nchini Tanzania ajulikanaye kwa jina la Kitale akimshirikisha msanii mwenzake ambaye kwa sasa ni marehemu, namzungumzia Sharo Milionea.

Wasanii hao kwa pamoja waliweza kutengeneza nyimbo nzuri na inayopendwa na wengi ijulikanayo kama HILI DUDE NOMA., Nyimbo hiyo imekuwa gumzo katika anga la muziki wa kitanzania. Kwa faida ya wapenzi wa Blog hii, mwasisi wa Studio ya Kwanza Records ni Amani Mwaipaja. Lengo kuu la studio ya Kwanza Records ni kusaidia vijana wa kitanzania kukuza vipaji vyao kupitia sanaa ya muziki hasa wasanii watokao mikoani.

Mpaka sasa, baadhi tu ya wasanii walioweza kutoka kupitia studio ya Kwanza Records ni pamoja na:
  1. Kitale na Sharo Milionea (jina la wimbo-Hili dude noma)
  2. Asha Boko (jina la wimbo-Kibonge Mnene)
  3. Joh Maker (Mshindi wa Fiesta Nyota akiwakirisha Mkoa wa Morogoro 2012)
  4. Mash J (Mshiriki wa Fiesta Nyota 2012 kutokea Morogoro)
  5. Afande Sele (jina la wimbo-Mashikolo Mageni)
  6. Ballet Wallet (jina la wimbo-Mr. President)
  7. Kenedy Masanja (jina la wimbo-Kamba Ndefu)
  8. Sesilia Saleko (jina la wimbo-Kwepa Uterezi)
  9. Sifuni Kwaya (Wamefanya albam nzima)
  10. Mao Thobias (jina la wimbo-Kinywa)
  11. Levina Stiven (jina la wimbo-Usikate tamaa)
  12. J-Zinga jina la wimbo-Kibena)
  13. Mycoel (jina la wimbo Rudi)
  14. Vent Skills (jina la wimbo-Stay away) 
  15. Swahili Genge (jina la wimbo-Red Card)
  16. Man Gao (jina la wimbo-Mama watoto)
  17. Man 2C (jina la wimbo-mzee wa kitaa)
  18. Jacca (jina la wimbo-mbiu ya mnyonge)
  19. Bon Face (jina la Wimbo-Bado mtoto)
  20. Mide Zoo
Kwa ujumla list ya wasanii waliopitia kwanza Records ni kubwa na inazidi kuongezeka kila kukicha.Studio ya Kwanza Records   ipo chini ya Producer Vent Skills na sasa Kwanza Records inamtambulisha kwenu Msanii Mycoel,Tafadhalini Mpokeeni Kwa mawasiliano piga 0653 361 070

photo



Tumo katika taifa lililogubikwa na maswali. Watu hawaoni tena nuru kwa maisha yao ya baadae. Mazungumzo ya watu barabarani, kwenye vyombo vya usafiri, vyombo vya habari, maofisini, sehemu za ibada, vijiweni na kwenye mikusanyiko ya watu hujiuliza tunakwenda wapi. Ugumu wa maisha umewafanya wengine wazikimbie familia zao huku wengine kwa kuchanganyikiwa wamejiua na kuua familia zao.


Hali ya kukata tamaa iliyoenea miongoni mwa wananchi wengi haitokani tu na matatizo peke yake wala maovu katika jamii. Kinachokatisha tamaa zaidi ni kuona viongozi walioapa kuwalinda wanananchi dhidi ya uovu wakicheka na uovu wenyewe na wakati mwingine wanakumbatiana na waovu hadharani. Mpaka sasa hakuna dalili kwa viongozi kumaliza kucheka 


Serikali sasa inakabiliwa na changamoto nyingi kutoka kila upande. Ni kama mfumo mzima wa utawala umesimama na Mungu ndiye ajuaye nini kitatokea kesho na keshokutwa ndani ya taifa letu.  Nchi inakabiliwa na tatizo kubwa la ukosefu wa ajira, umasikini uliokithiri, rushwa hususan kwenye mikataba ya kinyonyaji inayowanufaisha watu wachache katikati ya mamilioni ya watanzania. Uporaji wa rasilimali za taifa, mishahara midogo isiyoendana na hali ya maisha, kuporomoka kwa uchumi na huduma mbovu za kijamii ni baadhi tu ya dalili za ugonjwa hatari uliolikumba taifa.

(Hayo ni moja ya maelezo yaliyomo ndani ya kitabu changu cha shukrani ninachotarajia kukizinduwa mwishoni mwa mwezi wa tatu, kwa watakaohitaji nakala ya kitabu wasisite kunitafuta kupitia 0787 070707)

photo ,

Moja ya mambo ambayo kijana wa leo anaweza kujivunia ni namna anavyoweza kushiriki kikamilifu katika mambo ya siasa. ni vema tukakumbuka kuwa hata mwasisi wa Taifa hili Mwalimu Julius Nyerere wakati wa harakati za kudai uhuru yeye pamoja na wapigania uhuru wengi wa afrika walikuwa bado vijana, wenye nguvu na hali ya pekee katika kupigania haki za wanyonge.

Kama vijana hawashiriki kikamilifu katika mambo ya siasa, siku moja watakuja kujikuta wametawaliwa na mtu wa Hovyo, mpumbavu na mwendawazimu, nchi zote zilizo huru duniani viongozi wake huchaguliwa kupitia michakato ya kisiasa, Mwalimu Nyerere aliwahi kusema ili nchi iendelee inahitaji vitu vinne navyo ni ardhi,watu, siasa safi na uongozi bora.

Ni vema tukatambua pia kuwa siasa sio chafu kwa asili yake bali kuna viongozi wachafu ndani ya siasa, hawa ndio wanaoichafua taswira nzuri ya siasa

hivyo basi......Ukiona vijana kama akina Mnyika, Tundu Lisu, Halima Mdee, David Silindi, Kafulila,Joshua Nassari na wengineo wengi wanapigania haki za wanyonge, usipowaunga mkono,ukiwapinnga sasa, nawe ukiwa mzee utapingwa pia

photo

Kuna jambo tunaweza kujifunza kutokana na picha hii

photo


Mwanzoni mwa miaka ya tisini, chama cha mapinduzi kilianzisha mradi mchafu wa kisiasa kilipobaini uwezekano wa kusombwa na kimbunga cha uchaguzi. Kiliogopa kukataliwa na wananchi katika uchaguzi mkuu wa rais na wabunge wa mwaka 1995. Katika kutimiza malengo hayo, chama cha mapinduzi kilitafuta wataalam wa propaganda ili wabuni mradi wa hofu. Wakaeneza uzushi eti vyama vingi husababisha vita vya wenyewe kwa wenyewe.


Chama cha mapinduzi kikajaza watu hofu ya kupoteza maisha, kukatwa viungo, kupoteza ndugu na jamaa kwa vita iwapo watachagua upinzani. Walitoa sababu nyingi za kutochagua upinzani kwa kuinganisha na mauaji ya Rwanda, Burundi, sudan na Somalia.


Vyombo vya habari, hasa vya elektroniki vikasambaza hofu kwa kuonyesha picha za mauaji ya Rwanda na Burundi vikiwa na lengo la kuhujumu ustawi wa demokrasia na vyama vingi. Na  Kwakuwa wakati vyama vingi vikianzishwa watu wengi hawakuwa na uelewa wa kutosha juu ya mfumo wa siasa za vyama vingi, wengi wakalaani mfumo wa vyama vingi bila kujua kuwa vilianzishwa kikatiba


Walianza kuvuana magamba wenyewe kwa wenyewe wakasahau kuwa Kuvuana magamba kwa sasa ni sawa na kitendo cha kuweka maua mazuri juu ya kaburi la zamani. Maua hayo hayasaidii chochote kwa marehemu zaidi ya kufurahisha macho ya watu wengine wanaolitazama kaburi kwa nje.

Kwa wale watakaokumbuka, wakati ule chama cha wananchi CUF kilipokuwa ni chama kikuu cha Upinzani CCM walipandikiza chuki kwa propaganda kuwa CUF ni chama cha waislam hivyo kwa kiasi kikubwa wakafanikiwa kuigawa CUF na wakristo. Miaka michache baadae Chama Cha Demokrasia na maendeleo baada ya kuonekana kukubalika sana miongoni mwa watanzania CCM wakaja na propaganda ile ile waliyoitumia kwa CUF kwa kuiunganisha CHADEMA na ukristo na ukabila, ingawa propaganda hii haijawa na mashiko miongoni mwa watanzania wa leo lakini wapo baadhi ya watu ambao bado hawaelewi kama huo ni mchezo mchafu wa CCM................
(Maelezo haya yameelezwa kwa kirefu ndani ya kitabu changu cha shukrani)
  

photo ,

Mbunge mtarajiwa wa Morogoro mjini kupitia CHADEMA Bw. Amani Theophilus Mwaipaja ,anatarajia kuzindua KITABU chake tarehe 30/03/2013 mjini Morogoro,ambamo ndani yake kitakuwa mahususi kwa ajili ya SHUKRANI kwa wapenda maendeleo wote na wanaharati wote wa ukombozi wa wanyonge na  pia waliokuwa nae bega kwa bega katika uchaguzi uliopita. Katika uzinduzi huo anatarajia kuzindua na blog yake na mgeni rasmi anatarajiwa kuwa ni Kiongozi wa kitaifa wa CHADEMA. Kama unahitaji KITABU hicho ufanye mawasiliano mapema kwa simu: 0787 070 707 na 0714 559 910.

photo

Kutoka kushoto:Uhuru Kenyatta na William Ruto wakiteta Jambo katika kampeni zao za mwisho za uchaguzi ujao wa Kenya ,utakaofanyika jumatatu tarehe 4/3/2013 ,walitembelea mitaa ya Kapkatet, Bungoma na Homabay nchini Kenya ,wao wakiwakilisha kundi la JUBILEE.
Uhuru Kenyatta(gari la bluu)  na William Ruto (gari jekundu) wakiwa katika magari ya wazi katika kampeni zao za mwisho za uchaguzi ujao wa Kenya ,utakaofanyika jumatatu tarehe 4/3/2013 ,walitembelea mitaa ya Kapkatet, Bungoma na Homabay nchini Kenya ,wao wakiwakilisha kundi la JUBILEE.


Uhuru Kenyatta na William Ruto wakitaka kuyarudi mangoma katika kampeni zao za uchaguzi ujao wa Kenya ,utakaofanyika jumatatu tarehe 4/3/2013 ,walitembelea mitaa ya Kapkatet, Bungoma na Homabay nchini Kenya ,wao wakiwakilisha kundi la JUBILEE.
William Ruto akiteta Jambo katika kampeni za mwisho za uchaguzi ujao wa Kenya ,utakaofanyika jumatatu tarehe 4/3/2013 ,walitembelea mitaa ya Kapkatet, Bungoma na Homabay nchini Kenya ,wao wakiwakilisha kundi la JUBILEE.
Huu ni UMATI wa watu waliokuja kuhudhuria kampeni za JUBILEE katika mitaa ya Kapkatet, Bungoma na Homabay ,uchaguzi utakafanyika jumatatu tarehe 4/3/2013
Mwana dada akifurahia kampeni za upande wa JUBILEE ,akiwa amevaliwa vazi lenye jina la chama cha TNA ambacho Uhuru Kenyatta ndie anakiwania nacho urais wa Kenya Jumatatu Ijayo. Kwa hisani ya Wazalendo 25 Blog

photo


Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akipokea ujumbe maalumu kutoka kwa Rais Omar El Bashir wa Sudan ulioletwa na Mhe.Dkt.Nafie Ali Nafie ikulu jijini Dar es Salaam  Jana asubuhi.Picha na Freddy Maro-IKULU

photo