WANANCHI NI WAONGO VIONGOZI WAKWELI WATOKE WAPI?
Na Abdallah Mtibora
Ni rahisi sana kuelezea uongo kuliko kusema uongo ni nini. Wengine wanasema, Uongo ni kinyume cha ukweli, wengine wanasema uongo ni ile hali ya kusema ama kutenda kinyume na linalo takiwa kusemwa au kutendwa. Mimi nasema uongo ni hali ya kusema jambo lisilo la ukweli, kuahidi jambo ambalo halikutekelezwa kama lilivyo ahidiwa, au kutenda kinyume na makubaliano iwe ki maandishi, maneno au kisheria hivyo kwa mujibu wa maana yangu ya uongo, kutotimiza wajibu ni uongo (Niko tayari kusahihishwa, kwenye jitihada zangu za kupanua maana ya neno Uongo), ingawa si lengo la makala haya kujadili maana ya neno uongo.
Nasukumwa na dhamira ya mijadala mbalimbali kuhusiana na namna wanasiasa wanavyoshambuliana kuhusu uongo, sitajadili nani ni mkweli, ama nani ni muongo kwa maana naamini kila mmoja ana nafasi yake kuhusiana na suala la uongo.
Kuelekea uchaguzi Mkuu mambo mengi yatajitokeza,na mengine yameshaanza kujitokeza. Wanasiasa wenyewe kwa wenyewe watatuhumiana,kadhalika wananchi wataendelea kuwatuhumu wanasiasa kwa hadaa zao, na ahadi zisizotekelezeka.
Natambua uongo ni jambo ovu, hakuna dini yeyote inayoruhusu udanganyifu, lakini kadiri dunia inavyozidi kuzunguka ndivyo uongo unavyozidi kushamiri na unaelekea kurasimishwa siku zijazo, kama haujarasimishwa.
Nitatoa mifanomichache kuonesha ni kwa nini uwezekano wa kuondoa hadaa za kisiasa itatuchukua miongo kadhaa ikiwa uongo unaoonekana ni “mdogo” usipodhibitiwa kalaaniwa na kubezwa.
Mathalani mzazi ambaye ili mwanaye mdogo asilie wakati atakapo ondoka kwenda kwenye shughuli nyingine ziwe za kijamii au kiuchumi anavyomdanganya malaika wake. Tumekuwa tukisikia ama mama akisema ‘narudi sasa hivi’!, au usilie nitakuletea pipi. Lakini kinyume chake, pindi mama anaporejea aidha anakuwa amekawia kurudi, kinyume na ahadi yake au anarejea bila ile zawadi aliyo ahidi kwa mwanae (pipi)
Matukio ya kudanganywa kwenye ngazi ya familia yanaendelea kila uchao, mara mtoto aahidiwe nguo ya sikukuu, lakini ikifika siku ya siku anapewa visingizio lukuki, sasa najiuliza mtoto wa aina hii atauchukuliaje uongo. Je atauchukulia kama sehemu ya kutuliza maumivu ya mlalamikaji kama wafanyavyo baadhi ya wanasiasa wetu au atauchukulia kama uovu?, na je mzazi anaye mdanganya mwanaye ana “moral justification” ya kumchukia ama kumsema mwanasiasa aliyetoa ahadi ya uongo?.
Mfano mwingine ni wa mfanyibiashara anaye kwepa kulipa kodi, anatumia udhaifu wa mfumo wetu wa ulipaji wa kodi pamwe na udhaifu wa baadhi ya wakusanya kodi kukwepa kulipa kodi. Watu hawa ni maadui wa maendeleo ya nchi hii, ni maadui wa elimu ya nchi hii, ni maadui wa maendeleo ya kilimo chetu, ni maadui wa maendeleo ya kila sekta hapa nchini. Mfanyibiashara anaye toa takwimu za uongo ili alipe kodi kidogo anasema uongo, lakini inapotokea pengine kuna ahadi ya serikali kuhusu jambo lolote ambalo anafaidika nalo, na serikali ikachelewa kulitimiza, muongo huyu atakuwa wa kwanza kuinua kidole chake kumnyooshea muongo mwenzake ‘serikali’.
Mtu wa aina hii hawezi kukemea au kudai utekelezwaji wa ahadi ya serikali wakati yeye mwenyewe dhamira ya kutotimiza ahadi yake (kulipa kodi stahili) ingali inamsuta.
Tazama kiongozi wa taasisi ya kidini, ambaye Serkali yake inamsamehe kodi ili aweze kuihudumia jamii, lakini yeye anadanganya kwamba anatumia msamaha huo kwa lengo lililokusudiwa kumbe anautumia kwa mambo yake binafsi, mwisho wa siku serikali inapoteza asilimia 30 ya mapato yake, kwa vile serikali huongozwa kwa kodi, serikali inaposhindwa kutimiza wajibu wake kwa wananchi wale waongo waliotumia msamaha wa kodi visivyo, watakuja juu kuwalaumu waongo wenzao (serikali) kwamba inawadanganya.
Kadhalika, unaweza kuangalia uongo mwingine pale ambapo mkulima anapodanganya kwamba bidhaa zake ni nzuri kumbe katikati amejaza bidhaa mbovu, huu ni uongo, wanunuzi wa bidhaa za barabarani kama vitunguu, nyanya na viazi kwenye barabara itokayo Iringa, Dodoma, Morogoro na ile iendayo Arusha kutokea Dar watakuwa wanaelewa udanganyifu huo. Waongo hao, pia wanasimama kidete kuwalaumu waongo wenzao (Serikali) pale ahadi fulani fulani zinapokuwa hazijatekelezwa, inachekesha sana.
Kwa kweli uongo umetamalaki kila sekta, hebu fikiria chombo cha habari kinajiita chombo huru, lakini kuna baadhi ya watu ambao aidha ni washindani wa kibiashara wa mmiliki wa chombo hicho, au wanatofautiana ki itikadi, habari zao ambazo ni nzuri na za kimaendeleohaziwezi kutolewa kwenye chombo hicho, chombo kama hicho kinacho endelea kujinadi ati ni chombo huru, kinawadanganya wananchi. Sasa chombo hiki, ambacho kinawadanganya watu kwa jambo dogo kama hilo, kinaweza kusimamia ukweli?.
Ama tazama mfano wa muhadhiri wa chuo kikuu anayefundisha kwamba kilimo kinaweza kumuondoa mtanzania kutoka kwenye lindi la ufukara, lakini yeye anafungua mradi wa baa (bar) muhadhiri huyu sio muongo kweli?, ama muhadhiri wa sheria anayefundisha haki za binadamu, wakati yeye mwenyewe anazivunja kwa wanafunzi wake, ni neno gani linafaa kwa huyu muhadhir?, mnafiki au muongo?,na vipi kuhusu muhadhiri anayefundisha umuhimu wa viwanda vidogo vidogo, wakati yeye mwenyewe hayuko tayari kuanzisha kiwanda hata kimoja, achia mbali kuhamasisha wananchi wa eneo anapoishi kulingana na maana yangu ya uongo, mtu huyo ni muongo maana anatuambia kwamba jambo fulani ni jema, lakini yeye haliendei jambo hilo, jina analofaa kuitwa ni muongo, maana anasema jambo ambalo yeye mwenyewe haliamini.
Au chukulia afisa wa serikali ambaye amepewa dhamana ya kuwahudumia wananchi, anakula kiapo kuwatumikia wananchi bila upendeleo, choyo ama huba, lakini hatimizi ahadi yake, mtumishi wa aina hii anapocheleweshewa stahili zake anasimama imara kulaumu serikali kwa kutoa ahadi hewa, bila kukumbuka au kwa kujifanya hakumbuki uongo wake wakati wa utumishi wake.
Unaweza kuchukulia mfano wa baadhi ya waalimu wetu wa shule za serikali,ni kweli wanafanya kazi kwenye mazingira magumu, lakini nao wamekuwa hawatimizi wajibu wao ipasavyo, kwa kushindwa kutimiza wajibu wao na kudai stahili za kazi ambayo imefanywa chini ya kiwango nauchukulia kama ni udanganyifu, hivyo hata watetezi wa haki za walimu wakati mwingine wanashindwa kutetea uozo huo.
Mfano mwingine ni wa mwanafunzi aliyefaulu kwa njia za udanganyifu, aidha kwa kutumia udhaifu wa taasisi zetu za mitihani, ama kwa kununuliwa na shule yake, ili shule ipate umaarufu, mwanafunzi huyoni mungo kwani daraja alilopata si daraja lake stahiki, hata kama angeweza kulipata bila ya udanganyifu. Mtoto huyu ni muongo, tunatengeneza msomi muongo, ili aje akemee ukweli au abariki uongo?, na je atamnyima mwanaye pesa ili akanunue mtihani?, na je baada ya hapo atampongeza kwa kufaulu au kwa kuweza kudanganya bila kugundulika?.
Mfano mwingine wa uongo wa rejareja kwenye jamii yetu ni pale ambapo kondakta wa daladala anapowadanganya abiria wawahi viti kwenye gari ambalo limejaa, kondakta huyo ni muongo kama kiongozi ambaye anayewaahidi wananchi ujenzi wa barabara, il hali barabara zinajengwa kutokana na vipaumbele (Sina uhakika kama bado vipaumbele vinazingatiwa).
Ama chukulia mfano wa msaidizi wa ndani (House girl), ambaye muajiri wake (Sina uhakika kama wanaajiriwa) hamruhusu kupumzika ama kwenda kusalimia ndugu zake, ili aende kuwasalimia ndugu zake, inabidi ama adanganye kwamba anaumwa, au amefiwa, ni dharura hizo tu ndio zinazoweza kumtoa kwenye ngwamba ya kazi za ndani. Akisema ukweli haruhusiwi kabisa, ama msaidizi huyo inapotokea akavunja kikombe cha “muajiri” wake hawezi kuwa na utetezi wowote zaidi ya kutafuta uongo maridhawa ili “mshahara” wake uskatwe. Ni hivyo hivyo kwa mlinzi, dereva, ‘shamba boy’ na mlisha ngo’mbe.
Orodha ya uongo unaofanywa nchini kwa viwango tofauti tofauti ni ndefu, mathalani chukulia na wengi ni mashahidi kwenye magari ya abiria maarufu kama daladala mtu anatakiwa kwenye kikao cha kifamilia Gongo la mboto, yeye yuko Mbezi mwisho akipigiwa simu na wanandugu ili kujua alipofikia hawezi kuwaambia kwamba yuko Mbezi mwisho, baadala yake atasema yuko Tazara, ama Buguruni, pengine ili kuwapamoyo ndugu zake ya kwamba yuko karibu kufika kama ambavyo alikuwa akidanganywa angeletewa pipi ama aandazi ili asilie pindi mama yake alipokuwa akiondoka.
Mara nyingi tumekuwa mashuhuda juu ya uongo unaofanana na huo wa mkazi wa Mbezi mwisho, kuonesha kwamba uongo unakaribia kurasmishwa, abiria wamekuwa wakiishia kutabasamu ama kucheka tu. Hili limeendelea kuwa Taifa la wasema uongo kila idara, kila rika na kwenye kila taasisi, na viongozi wa dini wamekaa kimya wakisubiri serikali “iwadanganye” itafuta msamaha wa kodi kwa bidaa wanazoingiza, nao “waidanganye” serikali ati wataandamana hadi Ikulu kama msamaha huo utafutwa.
Hivi waziri anayemjibu mbunge mwenye hasira juu ya barabara ya jimboni kwake itajengwe lini, kwamba itazingatiwa kwenye bajeti ya mwakani ili ampunguze hasira na kumpa moyo mbunge huyo, anatofauti gani na mama aliyemdanganya mtoto ili asilie?, mkaazi wa mbezi ambaye anadanganya yuko tazara wakati angali anaoga ili awape moyo ndugu zake waendelee kumsubiri?. Ukitaka kujua jinsi uongounavyoelekea kurasimishwa, au umesharasimishwa kimyakimya jaribu kufikiria kama mheshimiwa waziri angejibu kwamba Serikali haina mpango wa kujenga barabara husika kwa miaka ya karibuni, au yule ndugu aliyeko Mbezi awaambie ndugu zake kwamba ndo kwanza anaoga, au msichana ambaye huna mpango wa kumuoa na uko naye kimapenzi utakapomwambia ukweli juu ya nia yako hiyo. Utagundua kwamba, jamii yetu inapenda lau idanganywe lakini iahidiwe kitu, hata kama hakitekelezeki.
Kwa baadhi ya mifano hiyo, na mingine ambayo wewe unayo, inashangaza kuona wanaobariki uongo wanaendelea kushangaa, wanapoambiwa uongo na waongo wenzao, hivi kama jamii yote ni ya wafugaji inakuwaje tushangae kuwa na kiongozi ambaye ni mfugaji?
Kwa vile uongo hauwezi kuendelea kuwa utamaduni wetu, na kwa kuwa uongo haupendezi hata mbele ya Macho ya Mungu (Kwa wanao amini uwepo wake), sisi kama jamii, bado hatujachelewa, tubadilike, tujifunze kusema ukweli hata kama ukweli huo ni mchungu, na jitihada hizo, zianzie ngazi ya familia, kwa kumwambia mtoto “nakwenda msibani nitachelewa kurudi usilie mtoto”, au kumwambia msichana uliyemtamani“ nina mihemko tu ya kimwili, na si kwamba nakupenda”, au waziri wa miundo mbinu anaweza kujibu “barabara flani haiwezi kujengwa mwaka huu au mwaka kesho, kwa vile barabara hiyo haina tija kiuchumi”, au ndugu wa jambazi aliyeuawa kwenye risala waseme “ndugu yetu kabla hajauawa tulikuwa tunaushuku utajiri wake” na kama kiongozi mbadhirifu akifariki, kwenye salamu za rambirambi tuseme “marehemu pamoja na sifa zote, pia alikuwa mbadhirifu, mjivuni, muongo na ngoni”.
.Tukifika hapo tutakuwa na sababu ya msingi ya kuwabeza viongozi waongo maana watakuwa sio sehemu ya jamii yetu, lakini kwa mwendo huu tulionao tunapowalaumu viongozi waongo wenzetu, labda tunataka viongozi wetu wadondoshwe na Mungu toka juu mbinguni.
Sisemi kwamba tusikemee uongo, lakini najiuliza hao waongo wametokea wapi?,je sio sehemu ya jamii yetu?, sisi tumesema uongo mara ngapi?, au tunapima uongo kwa mizania gani?, au tunaona kibanzi kwenye macho ya wenzetu ili hali nasi tuna boriti?. Waongo hawaepukiki, likini basi waongo wawe wachache wakweli wawe wengi, lakini bila hata ya utafiti,ni dhahiri jamii yetu imejaa waongo wengi na wakweli wachache, tubadilike, viongozi wa dini wakumbuke jukumu lao, wazazi pia na jamii nzima, vinginevyo hakuna anayestahili kukemea uongo, maana wakati mbunge anamlaumu waziri kwa kutowajibika na kudanganya, mbunge huyo huyo hajawajibika na amewadanganya wapiga kura wake jimboni, na waliodanganywa jimboni, pia wamezidanganya familia na hawawajibiki kwazo, na mzumguko unakwenda hivyo hivyo.
Tukemee sasa au tukae kimya milele, tuseme kweli maana kweli itatuweka huru.
Muandishi wa Makala hii Abdallah Mtibora ni mwanafunzi wa shule ya sheria “law school” anapatikana kwa simu namba 0717 - 714 728, e mail mtibora@hotmail.com